×

Our award-winning reporting has moved

Context provides news and analysis on three of the world’s most critical issues:

climate change, the impact of technology on society, and inclusive economies.

Mradi wa hali ya hewa unanuia kusaidia wakulima barani Africa

by Kizito Makoye | @kizmakoye | Thomson Reuters Foundation
Friday, 13 December 2013 11:53 GMT

Farmers in Mahembe village in Tanzania’s Morogoro region take part in community work to dig contour trenches, known as fanya chini, to prevent soil erosion caused by floods. THOMSON REUTERS FOUNDATION/Kizito Makoye

Image Caption and Rights Information

Effort aims to secure food security in Africa in the face of worsening climate change impacts

DAR ES SALAAM, Tanzania (Thomson Reuters Foundation) – Wakulima wanaokabiliwa na vipindi virefu vya ukame vikiambatana na mafuriko, wana matumaini kwamba mpango mpya wa kupambana na mabadiliko ya tabia nchi unaoanzishwa nchini Tanzania na Malawi, utawaondolea adha ya mazao hafifu.

Mpango wa huduma za hali ya hewa uliozinduliwa mwezi November na shirika la hali ya hewa la dunia, unatoa fursa kwa wakulima barani Africa wanaoweza kutumia ujuzi wa kisayansi kupambana na changamoto za hali ya hewa.

Ukifadhiliwa na mkopo wa dola million 10 kutoka serikali ya Norway, mradi huo wa majaribio unatarajiwa kuwapa mbinu maelfu ya wakulima nchini Malawi na Tanzania katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi yanayosababisha ukame na mafuriko.

Wakulima watafundishwa jinsi ya kuongeza ustahimilivu wa mazao na kutunza mashamba yao, kama vile matumizi ya mbegu stahimilivu, kubadilisha tarehe za kupand ili kukabiliana na mvua hafifu na upandaji wa wazao ya kukinga ili kuzuia magugu.

Mbinu nyingine ni pamoja na kuchimba mashimo kuzuia maji kupotea na uvunaji wa maji na umwagiliaji kukabiliana na uhaba wa maji. Wakulima pia watajifunza namna ya kupanda mimea ili kupunguza ongezeko la hewa ukaa.

“Kila mmoja wetu ameathirika na mabadiliko ya hali ya hewa. Ni matumaini yetu kwamba, iwapo wataalam watawezeshwa, watatusaidia sana kuepuka hasara zisizo za lazima.” Alisema Hamisi Ali, Mkulima kutoka Kijiji cha Matombo, Morogoro.

 “Huu ni mradi wa majaribio, hata hivyo, lengo ni kuona kwamba kila mkulima  nchini kote anajifunza mbinu hizi kupambana na mabadiliko ya tabia nchi.” Alisema Richard Muyungi mkurugenzi wa idara ya mabadiliko ya tabia nchi kwenye ofisi ya makamo wa rais wa Tanzania.

“Tumeichagua Tanzania kwa sababu ni nchi ya mfano kwa kadiri huduma za hali ya hewa na mabadiliko ya tabia nchi yanavyo husika,” alisema katibu mkuu wa shirika la hali ya hewa la dunia, Michael Jarraud.

Wakulima wa Morogoro ambao tayari wanakabiliwa na athari za mabadiliko ya tabia nchi wameiomba serikali ya Tanzania kutumia fursa hii kutoa mafunzo maalum ya namna gani tabia nchi inaathiri kilimo,kwa wataalam wa hali ya hewa na maofisa ugani wanaofanyakazi kwa karibu na wakuliama

 

 

Mpango huu wa kwanza unaoshirikisha mashirika mengi, unatarajiwa kuwezesha wakulima barani Africa kulinda shughuli zao zinazoathiriwa kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya tabia nchi. Kwa mujibu wa WMO mpango huo utaanza mwakani.

“Wakulima wengi hawana mbinu za kukabiliana na upungufu wa maji, kuzuia mmomonyoko wa udongo kwenye mashamba yao.” Alisema Robert Selasela, mkulima na diwani wa kata ya Kiroka. “Kama tukipata taarifa sahihi sina shaka tatizo hili litakuwa historia”

Wakulima wengi nchini Tanzania wanaathiriwa sana na mabadiliko ya hali ya hewa kutokana na kutegemea kilimo cha mvua. Sekta ya kilimo inachangia zaidi ya asilimia 30 katika pato la taifa. Tanzania ina zaidi ya hekta million 44 ya ardhi inayofaa kwa kilimo, hata hivyo ni hekta millioni 10 tu ndizo haswa inalimwa.

Kwa mujibu wa WMO, wakulima watapata fursa kupanga mikakati yao ya kilimo na masoko kulingana na taarifa za msimu ya hali ya hewa. Mradi huo pia utatoa fursa kwa wadhibiti wa majanga kutumia vifaa vya kisasa kujiandaa kwa hali ya dharura.

Serikali ya Tanzania inakisia kwamba, bila ya mipango stahimilivu dhidi ya tabia nchi, huenda  uzalishaji wa mahindi ukapungua kwa zaidi ya asilimia 16 kufikia mwaka 2030, ( hasara ya takribani tani million moja kwa mwaka) na  asilimia kati ya 25 had 35 kufikia mwaka 2050.

Omar Jaka, Mkulima wa mpunga, Morogoro, anataka shirika la hali ya hewa kupanua huduma zake za hali ya hewa kwenye simu za rununu ili iwafikie watu wengi.

“Watu wengi wanamiliki simu za mkononi siku hizi. Wakulima ni lazima wazifikie taarifa za hali ya hewa bila kikwazo kupitia simu za mkononi.

Mkurugenzi mkuu wa shirika la hali ya hewa, Agnes Kijazi, amesema matumizi ya taarifa za hali ya hewa ni muhimu ili kufikia dira ya maendeleo ya 2025 na azimio la kilimo kwanza - mkakati unaolenga kuleta mapinduzi ya kisasa katika kilimo.

 “Mpango huu ni fursa adhimu kwa kuwezesha upatikanaji wa taarifa,” alisema, “utatoa fursa kwa shirika la hali ya hewa kuhudumia wateja wake.”

Augustine Kanemba, mtabiri mkuu wa hali ya hewa wa TMA alisema mabadiliko ya tabia nchi huenda yakaathiri Zaidi uzalishaji wa chakula iwapo hali ya hewa itazidi kubadilika.

“Taarifa za hali ya hewa ni muhimu sana kwa wakulima, hasa wakati wa msimu mbaya ambapo kuna mavuno hafifu,” alisema.

Kwa mujibu wa Kanemba, huduma za hali ya hewa barani Africa hazipati pesa ya kutosha kwa kuwa serikali nyingi hazijatambua mchango wake kwenye maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Bara la Africa lingali kwenye hatari ya matokeo mabaya ya tabia nchi yanayoathiri uzalishaji kusababisha mafuriko na uharibifu wa pwani za bahari. Wataalamu wanaonya kwamba bila ya mbinu madhubuti za kustahimili huenda wakulima wengi wakapoteza ajira zao.

Henry Mahoo, mkufunzi wa uhandisi wa kilimo katika chuo Kikuu cha Sokoine mjini morogoro anasema kutokana na mabadiliko ya tabia nchi, rasilimali maji ingali inapungua katika maeneo mbalimbali ya nchi, matokeo yake, watu wanagombania maji

Kwa mujibu wa mahoo, mipango ya kustahimili mabadiliko ya tabia nchi ni lazima iwe na lengo la kupunguza hewa ukaa wakati huo huo kuongeza uzalishaji wa chakula.

Utafiti unaojulikana kama Economics of Climate Change in Tanzania, uliofadhiliwa na serikali mwaka wa 2011 unaonyesha kwamba ustahimilivu una nafasi kubwa kuzuia matokeo mabaya ya mabadiliko ya tabia nchi, hata hivyo, kiwango kikubwa cha pesa kinahitajika kuepuka upungufu uliopo.

Kwa mujibu wa utafiti huo, kiwango kinachokisiwa kujenga uwezo wa kuhimili ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi katika siku za usoni ni kati ya dola za kimarekani milioni 100 hadi 150 kwa mwaka.

Our Standards: The Thomson Reuters Trust Principles.

-->