Source: http://www.trust.org/item/20160713100045-407c4/


Use of this content is subject to the following terms and conditions: http://www.trust.org/terms-and-conditions/



Kampuni za umeme wa jua zapata mikopo kuangaza vijiji vya Tanzania


By Kizito Makoye | Wed, 13 Jul 2016 10:00 AM



DAR ES SALAAM (Thomson Reuters Foundation)—Kampuni ya ARTI Energy ilipoleta taa zinazotumia mwanga wa jua kijijini Kiromo  wilaya ya Bagamoyo miaka minane iliyopita, wenyeji walifurahi ila hawakujua iwapo watamudu kuzinunua.

 “ Nilizipenda sana taa zile, lakini sikudhani wakati huo iwapo ningaliweza kumiliki moja,” alisema Salum Ali mkazi wa Kiromo.

Ikiongozwa na Imani kwamba mwanga ni hitaji la muhimu kwa binadamu, kampuni hiyo  inayosambaza vifaa vya umeme wa jua iliamua kuuza taa hizo kwa mali kauli.

Kampuni hiyo inasema kwamba ilielewa kuwa  wakazi wengi vijijini wasingaliweza kumudu kununua taa hizo moja kwa moja kutokana na ukweli kwamba uwezo wao kifedha  ni mdogo.

Hata hivyo ndani ya miezi michache tu toka huduma hiyo ianzishwe  kwa kutumia mfumo wa  mali kauli, unaoruhusu wateja  kununua bidhaa kwa mkopo na kulipia baadaye, kampuni hiyo iliuza taa nyingi sana  na mfumo wa nishati jua  majumbani kwenye wilaya hiyo masikini.

Ali- ambaye angali anatumia taa ya umeme jua aliyonunua miaka minane iliyopita, anasema ingali ikifanya kazi vizuri.

“ Sina cha kulalamika, naitumia taa hii nyumbani na kwenye shughuli zangu za uvuvi,” alisema mvuvi huyo mwenye umri wa miaka 48.

 Mpango huo ambao sehemu ya mradi wa benki  ya dunia uliojulikana kama Lighting Rural Tanzania, uliotekelezwa kwa pamoja na  shirika la umeme vijijini yaani REA, uliwavutia mawakala wengi na wauza duka  waliopenda kuziuza taa hizo kwa niaba ya  kampuni ya ARTI.

 Mfumo wa mali kauli  unatumika sana vijijini kutokana na uaminifu wa wateja, na wauzaji na ushirikiano kati ya wauzaji na wasambazaji wa bidhaa.

 Ni kwa kupitia mfumo huu Kampuni ya ARTI Energy iliweza  kuleta taa ya umeme wa jua ya bei nafuu na kunufaisha zaidi ya familia  6000 kwenye wilaya hiyo kongwe.

Kwa mujibu wa  Shirika la Takwimu la taifa, ni robo tu ya watanzania wana huduma ya umeme. Huku mahitaji ya umeme yakiongezeka kwa kasi ya kati ya asilimia 10 hadi 15 kwa mwaka, serikali inasema familia nyingi vijijini huwa zinaachwa  katika shughuli mbalimbali za uchumi kutokana na kukosa umeme.

 Na huku umeme wa jua ukileta matumaini ya kuongeza idadi ya watu watakaopata huduma hii muhimu vijijini,  kampuni nyingi zinazojuhusisha na usambazaji wa bidhaa ya umeme jua  zinashindwa kupanuka kutokana na kukosa mtaji.