Source: http://www.trust.org/item/20140404223849-uszi7/


Use of this content is subject to the following terms and conditions: http://www.trust.org/terms-and-conditions/



Mwongozo Mpya wa Kilimo wasaida wakulima wa kiislamu barani Africa kukabili hali ya mabadiliko ya tabianchi


By Pius Sawa | Sun, 6 Apr 2014 10:00 PM



NAIROBI (Thomson Reuters Foundation) – Waislamu barani Africa ambao hulima katika maeneo yasiyo na rotuba nyingi, wametoa kijitabu ambacho ni mwongozo wa kilimo endelevu ili kuwawezesha mamilioni ya wakulima wa kiislamu barani wanaokabiliwa na tishio la chakula kutokana na mabadiliko ya tabianchi.

Mwongozo huo unafafanua masuala ya kilimo hifadhi ambacho kinazingatia kupata faida ya mazao mengi huku mazingira yakihifadhiwa.

Takriban waislamu milioni 248 barani Africa wanakabiliwa na mabadiliko ya tabianchi kwa sababu wengi wao wanaishi katika maeneo yenye ukame, huku kilimo kikiadhiriwa na ukosefu wa mvua na mafuriko.

“Tuna mamilioni ya watu wanaoshinda bila chakula kwa sababu misitu imeharibiwa, wanyama wamepungua, udongo umeharibiwa na mazingira kwa ujumla yameharibiwa,” alisema Abdulghafur El-Busaidy, ambaye ni mwenyekiti wa baraza kuu la kiislamu nchini Kenya SUPKEM.

Mwongozo huo unaojulikana kama “Islamic farming: A tool for conservation agriculture,” unajumuisha mafunzo ya kitabu kitakatifu cha kurani yenye kuhimiza namna ya kulinda ardhi na kina maelezo ya namna ya kulima bila kuharibu mazingira.

Ni mradi ambao unajumuisha masharika matatu ambayo ni shirika la uingireza la msaada linaloshirikisha makundi ya kidini katika kustawisha miradi ya kimazingira, Alliance of Religions and Conservation (ARC), Baraza kuu la kiislamu nchini Kenya, SUPKEM na Shirika la kimataifa la wanawake wa kiislamu Global One 2015.

USHAWISHI

Susie Weldon kutoka shirika la ARC, alisema kuwa wazo la waislamu kutaka kuwa na mwongozo wao wa kilimo hifadhi iliibuka mwaka 2012 jijini Nairobi wakati wa mkutano wa mashirika ya kidini. Wakuu wa Kiislamu waliokuwa katika mkutano huo walifurahishwa na kitabu cha wakristu chenye maelezo juu ya kilimo cha kidini, yaani, “Farming God’s Way”.

Kitabu hiki pamoja na vitabu vingine vyenye kuzingatia mafunzo ya kibibilia katika kilimo, vilikuwa na mafunzo ya nguvu miongoni mwa wakristo kwa sababu viliwazungumzia kama wakristo, alisema Weldon.

Kulingana na Husna Ahmad, mkurugenzi mkuu wa shirika la Global One 2015, mwongozo huu mpya unaangazia suala la kiislamu la “Rizq”, maanake riziki, na unazingatia mafunzo ya kiislamu ambayo ni kupanga, kuandaa, kupanda, kugawa, kulinda na kuzalisha.

Weldon alisema muongozo huu ni mwanzo tu wa vuguvugu la dini mbalimbali kushiriki katika kudumisha kilimo barani Afrika.

“Tunaamini kuwa huu utakuwa mwanzo wa mashirika ya kidini kuwasaidia wakulima kukuza chakula cha kutosha huku mazingira na udongo ikihifadhiwa, alisema Bi. Weldon.

Kwa miaka kadhaa sasa, Hajji Ahmed Muguluma kutoka Uganda amekuwa akijaribu kufanya kilimo hifadhi kwenye shamba lake la ekari 15, lakini hakuwa na mwongozo.

“Hiki ni chombo ambacho kimeletwa na Mwenyezi Mungu. Wakulima wengi na hata sisi hatukujua ni wakati gani na ni namna gani ya kufanya,” alisema.

Muguluma, ambaye pia ni mwenyekiti wa mtandao wa kidini wa mazingira nchini Uganda, Uganda Faith Network on Environment Action, anasema kuwa shirika lake limetenga  ekari 50 katika maeneo tofauti ili kuwafunza wakulima jinsi ya kudumisha kilimo hifadhi ambapo, kwekwe shambani hazichomwi kwa moto, na miti hupandwa ili kuhifadhi mazingira na pia kuhifadhi maji mchangani kwa kufunika udongo kwa majani.

Idadi ya watu nchini Uganda imeongezeka mara nne tangu nchi hiyo kupata uhuru mwaka 1962, na vijana wengi wamehamia maeneo ya mijini ili kutafuta ajira. Kulisha nchi nzima bila kuzingatia kilimo hifadhi ni changamoto kubwa, alisema Muguluma. Idadi kubwa ya misitu imepotea na hivyo kusababisha tatizo la mmomonyoko wa udongo.

Lakini  Husna Ahmad wa shirika la  Global One 2015 alisema kilimo cha awali cha waislamu kilikuwa bora katika kuhifadhi na kutunza ardhi.

“Mwongozo huu ni kuwakumbusha waislamu kuwa ili kuwa na usalama wa chakula, ni lazima wawe karibu na mafunzo ya Allah. Mwamini Allah, na mjaribu kuwa wakulima bora ndio ujumbe mkuu katika kijitabu hiki,” alisema.

Jane Oyuke, kutoka wizara ya kilimo nchini Kenya alikiri kuwa aina hii ya kilimo sio suala geni barani Afrika.

Alisema wazo hilo lilibuniwa mwaka 2008 na muungano wa Afrika ili kukabili maafa ya mabadiliko ya tabianchi na mashirika ya kiafrika kama vile COMESA, SADC na muungano wa Afrika mashariki yameanza kuitekeleza.

Alisema kubadili mawazo ya wakulima ni changamoto kubwa ambapo wakulima wanadhani kuwa kilimo hifadhi ni jinamizi ilhali ni njia rahisi ya kupata mazao mengi bila kutumia gharama nyingi za kunua mbolea na pia hupunguza muda wa kuwa shambani.

Kijitabu hiki sasa kimetafsiriwa katika lugha ya Kiswahili.