×

Our award-winning reporting has moved

Context provides news and analysis on three of the world’s most critical issues:

climate change, the impact of technology on society, and inclusive economies.

Huku mafuriko yakitishia, Tanzania yapania kujenga jiji bora

by Kizito Makoye | @kizmakoye | Thomson Reuters Foundation
Monday, 21 July 2014 12:15 GMT

A motorcyclist negotiates his way through a flooded road along Bibi titi Mohamed street in Dar es Salaam, following a heavy downpour in March 2014. THOMSON REUTERS FOUNDATION/Zuberi Musa

Image Caption and Rights Information

Can planning for climate change help Dar es Salaam become a better city as well as a bigger one by 2036?

DAR ES SALAAM (Thomson Reuters Foundation)— Dar es Salaam, jiji kubwa la kibiashara Tanzania-miongoni mwa jiji zinazokua kwa kasi barani Africa-limechora upya mpango mji wake na kujaribu kuwa jiji bora zaidi litakaloweza kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi, na siyo jiji linalokua holela na kuzongwa na mafuriko.

Mpango huo, wenye kuakisi mwaka 2036, unalenga kulibadili jiji la takribani watu milioni 4.5 na kupendekezwa kwa mamlaka ya maendeleo ya jiji itakayo simamia mipango na maendeleo ya miundomsingi, ikiwemo usafiri na huduma za jamii.

Unatoa wito kuwe na juhudi za kuingiza mipango ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kweye sera za maendeleo ya jiji, mathalani ujenzi wa mifereji ya maji ya mvua katikati ya jiji linaloathiriwa sana na mafuriko, pamoja na kuhamisha wakazi wa mabondeni.

Mamlaka pia itakuwa na nguvu za turufu kupinga maamuzi ya mipango miji yaliyofanywa na halmashauri za manispaa yasiyoendana na sera za matumizi ya ardhi jijini.

Said Meck Sadick, Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam aliiambia Thomson Reuters Foundation kwamba serikali inataka kuona Dar es salaam inakuwa na kuwa jiji kubwa lenye taasisi za kisasa, viwanda na miundomsingi itakayo vutia wawekezaji na kupokea ongezeko la watu.

Mafanikio ya mpango huu, hata hivyo, yatategemea utekelezaji wa taratibu na kuzuia ujenzi holela wa majengo kwenye maeneo hatari, Sadiki alisema.

Dar es Salaam inayokuwa kwa kasi sana, inazalisha asilimia 40 ya pato la taifa hata hivyo iko hatarini kutokana na tishio la mabadiliko ya tabia nchi, kama vile mafuriko, kuongezeka kina cha bahari, mmomonyoko wa udongo, upungufu wa maji na magonjwa yanayosababishwa na wadudu.

WATU MILIONI 10 KUFIKIA 2040

Kwa mujibu wa utafiti wa serikali uliofanyika 2011, Dar es Salaam iko mbioni kuwa jiji lenye watu zaidi ya million 10 mpaka kufikia 2040. Hata leo, takriban watu 140,000 wanaishi mabondeni kwenye hatari ya mafuriko, miongoni mwao 31,000 wakiwa katika hatari kuu.

Huku idadi wa yatu wanaoishi kwenye makazi duni yasiyo na maji wala huduma muhimu ikiongezeka, Dar es salaam ni kielelezo cha changamoto za kupambana na ukuaji wa miji, umaskini na majanga ya asili kwa mujibu wa wataalam wa ECLEI, mtandao wa zaidi ya majiji elf moja unaofanyakazi zinazohusiana na maendeleo endelevu na mambo ya ustahimilivu.

Serikali inakisia kwamba, karibu asilimia 70 ya wakazi wote Dar es Salaam wanaishi kwenye makazi duni yaliyobanana yaliyopo pembezoni mwa jiji na yenye kuathiriwa mno na mafuriko.

Kwa mujibu wa ripoti ya Resilent Cities Congress Secretariat, kufanya maendeleo mbali na maeneo hatarishi ni miongoni mwa njia nzuri za kudhibiti gharama itakayoweza kuletwa na mabadiliko ya hali ya hewa hapo baadaye.

Hata hivyo, Silvia Macchi, mkufunzi na mtaalam wa mipango miji, chuo kikuu cha Sapienza huko Italy, na ambaye amefanya kazi zinazohusiana na mradi wa mabadiliko ya tabia nchi Dar es salaam, alisema mpango mpya wa jiji hauangazii vya kutosha juu ya mipango ya baadaye ya namna ya kukabiliana na tishio la mabadiliko ya tabia nchi na unakosa, “fursa ya kuunda upya sera ya mji na jiji lenyewe” ili kujenga ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi.

“Ingawa mabadiliko ya tabia nchi yamegusiwa kidogo kama ni dira muhimu kwenye mkakati wa maendeleo ya jiji unaoandaliwa, hamna chochote kilichoeleza namna ya kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi kama vile mpenyo wa maji chumvi kwenye uwanda wa pwani” na ugavi wa maji jijin I,” alisema kwenye barua pepe.

Upungufu huo, “pengine unaotokana na ugumu wa matatizo yanayolikabili jiji la Dar es Salaam,” alisema. Hata hivyo, maofisa walioupanga mji, “hawakubadili mtazamo wao wa namna wanavyoliangalia jiji hili,” alifoka.

Mabadiliko ya namna hiyo ambayo yametokea kwa muda mrefu tayari, yanaathiri watu wanaoishi pwani, wanaojaribu kukinga maji ya mvua kwa kuwa maji ya kisima hayanyweki tena kutokana na chumvi, na vile vile wanajaribu kutafuta vyanzo mbadala vya kipato ili kuweza kukabiliana na changamoto za kimazingira.

Mpango mpya wa jiji ni lazima utambue kwamba, “mambo hayo yanawakilisha rasilimali muhimu sana ili kupanga ustahimilivu,” alisema.

KUHAMISHWA KUTOKA KWENYE MAKAAZI DUNI

Tatizo moja linalokabili maafisa Dar es Salaam na majiji mengine makubwa, taarifa ya ICLEI inasema, ni namna ya kutekeleza sera za matumizi ya ardhi mijini mahali ambapo wengi huishi kwenye makazi yasiyo rasmi.

Kama sehemu ya mpango wa ustahimilivu dhidi ya tabia nchi, unaohusisha ujenzi wa ukuta wa bahari, upandaji wa mikoko na uwekaji wa mifereji ya maji, serikali imehamisha wakazi 654 ambao nyumba zao zilizungukwa na maji mwaka 2011. Walipewa viwanja vyenye ukubwa wa meta za mraba 100 takribani kilomita 35 kutoka jiji la Dar es Salaam.

Kwenye mahojiano na Thomson Reuters Foundation, Aziza Ali, mkazi mmojawapo aliyehamishwa, alisema ilikuwa ni habari njema kupata kiwanja hata hivyo hawezi tena kuendelea na kazi yake ya upishi kwa kuwa amehamia mbali sana na waliokuwa wateja wake.

“Usafiri ni kikwazo kikubwa sana hapa. Siwezi kulipa 3000 ($2) kama nauli kila siku kwenda mjiji, alilalama.

Familia yake ingali inaiishi kwenye hema lililotolewa na serikali walipohamia mwaka 2011.

“Nilipewa mifuko 100 ya saruji na mabati Rais alivyokuja kututembelea, lakini kwa kuwa sina pesa za kujenga nyumba niliishia kuuza vifaa vya ujenzi kulisha familia yangu,” alisema Aziza.

Sadick alisema jitihada za kuhamisha wakazi wa mabondeni zinakwamishwa kwa sababu ya ukosefu wa fedha na maeneo ya kuwapeleka. Watu wengi hata hivyo, wanapenda kuishi katikati ya jiji kwenye huduma za jamii na shughuli za uchumi, alisema.

Ikiwa sehemu ya mpango mpya, mamlaka za jiji zinatekeleza mradi wa mamilioni ya dola ya mabasi yaendayo kazi, unaolenga kuleta mabasi yaendayo kasi kuwaleta watu wanaoishi pembezoni mwa jiji kazini kila siku.

Kizito Makoye ni mwandishi mwandamizi aliyepo Dar es Salaam, Tanzania. Anaandika kuhusu mabadiliko ya tabia nchi na mambo ya utawala.

Our Standards: The Thomson Reuters Trust Principles.

-->